By Khadija Mbesa
Taarifa ya Benki ya Dunia, kuhusu Tangazo la Serikali ya Tanzania kuhusu Upatikanaji Sawa wa Elimu kwa Wasichana Wajawazito na Kina Mama Vijana.
Benki ya Dunia, hapo jana, imetoa taarifa ifuatayo kuhusu tangazo la Serikali ya Tanzania kuhusu kupanua na kuhakikisha upatikanaji wa elimu rasmi kwa wasichana, hasa wanafunzi wajawazito na kina mama vijana katika shule za serikali:
Benki ya Dunia inakaribisha tangazo la Serikali ya Tanzania la kuondoa vikwazo vya upatikanaji wa elimu, vikiwemo vile vinavyozuia wasichana wajawazito au kina mama vijana kwenda shule rasmi. Uamuzi huu muhimu unasisitiza dhamira ya nchi kusaidia wasichana na wanawake vijana na kuboresha nafasi zao za kupata elimu bora.
Tanzania sasa itawaruhusu wasichana wenye umri wa miaka 12 hadi 19 walioacha shule kwa sababu ya ujauzito kurejea shuleni baada ya kujifungua, waziri wa elimu alisema hapo Jumatano, huku akitia kituo kamili, marufuku ya kurudi kwa wanafunzi kama hao. jambo ambalo limeshutumiwa na makundi ya kutetea haki za binadamu kuwa ni za kibaguzi.
Hatua hiyo imekuja baada ya wizara hiyo kutoa tangazo la mwezi Juni kuwa wanafunzi wanaoacha shule za sekondari wakiwemo wasichana waliopata mimba wakiwa shuleni wataweza kurejea masomo yao katika vyuo mbadala.
“Serikali imeamua kuwa, wanafunzi wote wanaoacha shule kwa sababu mbalimbali watapewa fursa ya kurejea shuleni,” Joyce Ndalichako, waziri wa elimu, sayansi na teknolojia aliuambia mkutano wa waandishi wa habari katika mji mkuu wa utawala Dodoma.
Kwa mujibu wa Benki ya Dunia, zaidi ya wasichana 120,000 huacha shule kila mwaka nchini Tanzania, na idadi ya 6,500 kati yao wanatokana na ujauzito au kupata watoto mapema.
Haya yote ni baada mashirika ya kutetea haki za binadamu yamekosoa marufuku ya Tanzania ya kuwarejesha wanafunzi katika elimu rasmi baada ya kujifungua.
Benki kuu inatarajia kutoa miongozo itakayowawezesha wasichana wajawazito na kina mama vijana kuendelea na masomo na itasaidia utekelezaji wake kupitia ushirikiano wa Serikali ya Tanzania katika sekta ya elimu. Kuifanya elimu kuwa bora, salama, na ipatikane zaidi ni muhimu ili kuendeleza maendeleo ya kijamii na kiuchumi ya Tanzania.