By Khadija Mbesa
Wakati kila mtoto anaonekana yupo shuleni ama nyumbani mwao, utamwona Mtoto wa miaka 12 amekaa chini ya mti katika makaburi ya al-Faluja, kusini magharibi mwa kambi ya wakimbizi ya Jabalia kaskazini mwa Gaza, akijikinga na miale ya jua kali, huku akisubiri wageni wa makaburi wafike ili awape huduma kadhaa kwa malipo kidogo ya fedha.
Nyakati za mchana, Hassan (jina la mtaani) anamwona mtu aliyekuja kuzuru kaburi la mtu wake. Anachukua chupa za maji za plastiki alizojaza kutoka kwa maji ya bomba kwenye makaburi na ufagio, na kumfuata mgeni kaburini. Mvulana anafagia jiwe la kaburi na kumwagilia mimea inayoizunguka maji, kisha anamuomba mtu huyo shekeli moja au mbili, hiyo ni sawa na senti 31 hadi 61 za Amerika.
Hassan ni mmoja wa watoto wengi ambao walianza kuombaomba katika makaburi Kwa sababu ya kuongezeka kwa viwango vya umasikini katika eneo lililouzingira. Kulingana na Wizara ya Maendeleo ya Jamii huko Gaza, ukosefu wa chakula katika Ukanda wa Gaza umefikia asilimia 70, wakati umaskini na kiwango cha ukosefu wa ajira umefikia karibia asilimia 75 mnamo 2019.
Hassan pia huweka tope linalotumika kujaza mapengo wakati wa mazishi, kwa malipo ya pesa kutoka kwa familia ya marehemu au mkurugenzi wa mazishi, Jaber kwa shekeli tano ambayo ni dola moja na senti hamsini na tatu za merikani. Hassan anasema kuwa yeye haogopi wafu kamwe kwani walio hai hutisha Zaidi, hivyo yeye hubaki makaburini hadi jua linapozana.
Hassan ana dada mmoja na kaka saba, alilazimika kuacha shule akiwa kwa darasa la nane kwa sababu ya kiuchumi kwa hivyo omba omba makaburini ama kufanya kazi ili kupata fedha ndio imekua suluhisho lake.
Hii ni hadithi ya Hassan tu ila kuna Watoto wengi ambao wanaomba omba makaburini ama kufanya kazi ili kusaidia familia yao, kutokana na vita, Watoto wengi wamepoteza wazazi wao, hili likiongeza asilimia ya juu ya ufukara Gaza.
Maisha ya Watoto hawa yamekuwa ya kusikitisha mno kwani wao wakimwona mtu amekuja kuzuru makaburi basi humkimbilia na chupa ya maji na ufagio, wakiwa tayari kuwasafishia makaburi ya watu wao na kuyanyunyizia maji, wakati watu wengine huwapatia angalau shekeli moja, wengine hawawapatii hata ndururu.
Kutengwa na familia, yani talaka, matumizi mabaya ya dawa za kulevya au kutiwa mbaroni kwa wazazi pia kunachangia pakubwa pa kuzaliwa kwa Watoto omba omba. Watu wengi hukosa kuelewa kwamba, kufanikiwa au kuteseka kwa mtoto kunategemea na malezi ya mzazi wake.

Kunyimwa kwa malezi bora kwa hawa Watoto kutaelekeza Watoto hawa kuiga tabia mbovu kama vile, wizi, kuwa wadanganyifu, kuwa na maneno makali na hata kujiingiza kwa vita.
Ruba al-Bitar, afisa wa ulinzi wa watoto katika Wizara ya Maendeleo ya Jamii anasema kuwa maswala ya kisaikolojia kama wasiwasi, mafadhaiko, ndoto za kutisha, kutengwa na kuingiliwa, kwa sababu ya kutumia siku zao katika mazingira yaliyotengwa kwenye makaburi, ni kawaida kati ya watoto. Aliongeza, “Waombaji wa watoto wanakabiliwa na udhalimu zaidi kuliko wengine kwa sababu wanaomba katika eneo moja, ambalo mara nyingi hutembelewa na watu wazima ambao ni watumiaji wa dawa za kulevya na wezi wapotovu.”
Omba omba haidhuru afya ya mtoto tu bali afya ya akili pia, Watoto hawa wananyimwa Faraja, mapenzi ya kifamilia na bega la kutegemea, badala yake wanakabiliwa na ulimwengu huu mkali bila ya kuwa na mtu wa kumwendea.
Watoto hawa wanalazimika kutupilia mbali utoto wao na kujitwika gurudumu la majukumu.
Mtafiti wa uchumi Hassan al-Radih ana mapendekezo ya kutoa sheria au kanuni za kuhalalisha utumikishwaji wa watoto na kuombaomba, kuunda idara maalum katika Wizara ya Maendeleo ya Jamii inayolenga kupunguza idadi ya ombaomba watoto na kuwapeleka katika kituo cha ukarabati, kuwapa fursa za kazi zinazostahili umri, kukuza dhana. ya kazi na uzalishaji.
source, https://www.al-monitor.com/originals/2021/07/gazan-children-wander-cemeteries-pennies