By Martha Chimilila
Mkazi wa kijiji cha Ndumbwe, Wilaya ya Mtwara nchini Tanzania, anayejulikana kwa jina la Hamis Mmalala amemchoma vidole moto mtoto wake anayeitwa Bashiru mwenye miaka 10. Kitendo hiki kilitokea baada ya kumtuhumu mtoto kuwa ameiba shilling 1,000 iliyoandaliwa kwa ajili ya kununua vitafunwa.
Bwana Hamis Mmalala alizungumza na mwandishi wa gazeti la Mwananchi digital aliyefika nyumbani kwake ili kumhoji ‘niliwasha moto kwa nia ya kumtisha mtoto ili aache vitendo vyake vya udokozi sikuwa na lengo la kumuunguza’. Aliongeza kwa kusema;
“Mtoto aliungua kwa bahati mbaya na kusema kuwa huyu mtoto ana tabia ya udokozi hata anaiba unga na kuficha. Kuna siku aliiba mtama, nilikuwa namtisha kwa bahati mbaya nikamuunguza mkono”
“Sikuwa na nia mbaya na kama ningetaka kumdhuru basi ningemdhuru siku nyingi zilizopita ila nilikuwa namtishia tu,na sikutegemea moto ungewaka. Najua nilichokifanya sio sawa, ndo maana ninasema ni bahati mbaya”
Mtoto Bashiru alisimulia yafuatayo huku akionyesha vidole alivyounguzwa;
“Baba alinipeleka nyuma ya nyumba, alinifunga nyasi na kuwasha moto. Alifanya hivyo baada ya kunishtumu kuwa nimeiba pesa (shilling 1,000). Nililia sana lakini hakuacha, baadae aliuzima na kuniwekea dawa, nilishuhudia maji yakitoka katika vidole alivyoniunguza” aliongeza kwa kusema yafuatayo:
‘Inapofika muda wa kula huwa nakaa pembeni, wananikatia matonge ya ugali na kuniwekea kwenye kiganja ndiyo nakula. Siwezi kufanya chochote nimeungua vidole vinne vya mkono mmoja na kidole kimoja kwa mkono mwingine. Kila kitu nasaidiwa na watu’
Bwana Hamisi Mitandi, ambaye ni Mwenyekiti wa Kitongoji alisema kuwa;
“Nilichelewa kupata taarifa ya tukio hili, laiti ningepata taarifa mapema ningelifanyia kazi. Nimesikitishwa na tatizo alilolipata mtoto huyu, ninamfahamu mtoto huyu kwa muda mrefu na sijawahi kumuona au kusikia akifanya tukio kama hili”
“Huyu mtoto anahitaji malezi mazuri na muongozo ili aweze kuwa msaada katika jamii hapo baadae. Hili ni tukio la kwanza la ukatili kuwahi kutokea na nitahakikisha mtoto anapata matibabu”
Bwana Mark Njera, Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Mtwara, alitoa ufafanuzi wa tukio hili na kusema kuwa kuna kesi mbili za watoto kufanyiwa vitendo vya kikatili na wazazi wapo chini ya ulinzi.
“Vyanzo vya matukio haya ni vitendo vya ajabu kama mtoto wa kwanza alikula ugali na nyama na wa pili aliiba shillingi 1,000. Hii siyo sahihi na elimu kwa jamii inapaswa kutolewa Ijapokuwa tumezungukwa na jamii maskini”